JARIDA LA MNYAMPALA https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala <p><strong>Jarida la Mnyampala (JM)</strong> ni jarida la kitaaluma lililopo chini ya idara ya Kiswahili ya Chuo Kikuu cha St John’s cha Tanzania. JM limesajiliwa na Maktaba Kuu ya Taifa mwaka 2019 na kupewa namba ya usajili ISSN 2683-6440 (nakala ngumu [print]) na e-ISSN 2683-6432 (nakala tepe ya mtandaoni [online]). Jarida limejikita katika uchapishaji wa makala za Fasihi, Isimu na Utamaduni wa Kiswahili. Hivyo basi, waandishi, watafiti na wapenzi wa Kiswahili wanakaribishwa kuchapisha makala katika jarida hili. Makala zote zitumwe kwa mhariri mkuu kupitia baruapepe <strong>jaridalamnyampala@sjut.ac.tz.</strong></p> en-US jaridalamnyampala@sjut.ac.tz (Dkt. Shadidu A. Ndossa) jkungura@sjut.ac.tz (Johnkenedy kungura) Tue, 05 Oct 2021 00:00:00 +0000 OJS 3.3.0.8 http://blogs.law.harvard.edu/tech/rss 60 TATHMINI YA TAFSIRI YA JALADA LA KITABU: MIFANO KUTOKA TAFSIRI YA THE BLACK HERMIT (THIONG`O, 1968) NA KIFO KISIMANI (MBERIA, 2001) https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/7 <p align="justify">Lengo kuu la tafsiri ni kufanikisha mawasiliano kwa sababu hadhira lengwa haijui lugha wala utamaduni chanzi. Hivyo, mfasiri anapaswa kuwa mwaminifu kwa kulinda ukweli na ufasaha wa ujumbe wa matini chanzi katika matini lengwa. Ujumbe huo hubebwa na vipashio mbalimbali (maneno, virai, sentensi na aya) ambavyo mfasiri hana budi kuvizingatia. Aidha, mfasiri huzingatia vipengele vya lugha na masilugha vilivyomo katika jalada la tafsiri ili aweze kuandaa jalada la matini lengwa linaloendana na ujumbe wa jalada la matini chanzi. Hii ni kwa sababu jalada hubeba maana na ujumbe ulio kamili kwa kutumia lugha na masilugha. Hivyo basi, makala hii imetathmini tafsiri ya jalada la tafsiri ya tamthiliya ya The Black Hermit iliyoandikwa na Ngugi wa Thiong`o (1968), kisha ikatafsiriwa kama Mtawa Mweusi na Ngugi wa Thiong`o (1970) na tamthiliya ya Kifo Kisimani iliyoandikwa na Kithaka wa Mberia (2001) na ikatafsiriwa kama Death at the Well na Khalfan Kasu (2011). Tathmini imefanywa kwa kuchunguza kufanana na kutofautiana kwa tafsiri za majalada kati ya matini chanzi na matini lengwa. Makala hii imeongozwa na Nadharia ya Usawe wa Kidhima iliyoasisiwa na Nida (1964). Data imekusanywa kwa kutumia mbinu ya usomaji matini. Uchambuzi wa data hiyo umetumia mbinu linganishi na mkabala wa kitaamuli. Hatimaye, makala imebaini kuwa, licha ya vipengele kadhaa kufanana, bado kuna tofauti zinazojitokeza katika tafsiri hizo. Jambo hili linasababisha kutowiana kwa baadhi ya maudhui ya MC na ML. Hivyo, makala inapendekeza kwamba si kila jalada lazima litafsiriwe. Kutafsiriwa ama kutotafsiriwa kwa jalada la kitabu kunategemea muktadha wa tafsiri husika.</p> Haule Jacob Copyright (c) 2021 https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/7 Tue, 05 Oct 2021 00:00:00 +0000 MAUDHUI KATIKA NYIMBO ZA TOHARA ZA WAMASAABA NCHINI UGANDA https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/13 <p align="justify">Makala hii inaeleza maudhui mbalimbali yanayopatikana katika nyimbo za tohara za Wamasaaba nchini Uganda. Kulingana na wataalamu mbalimbali wa fasihi, maudhui ni mambo muhimu yanayopatikana katika kazi za sanaa. Nyimbo za tohara ni miongoni mwa kazi za sanaa ambazo hutekelezwa na binadamu. Katika makala hii, mwandishi anazingatia nadharia ya ethnografia na utendaji ambayo inalenga watu na ubunifu wao. Kwa kuzingatia nadharia hii, mwandishi anaeleza jinsi wanasanaa mbalimbali wanavyobuni nyimbo ili kuwasilisha mawazo yao. Mwandishi anafanya hivyo kwa kurejelea angalau mfano mmoja wa nyimbo hizo kwa kila maudhui. Mwandishi amepanga maudhui hayo kulingana na utaratibu wa utendaji wa nyimbo hizo za tohara. Kutokana na jambo hili, mwandishi anaangalia mambo mbalimbali katika utekelezaji wa tohara kwa sababu nyimbo hizo huambatana na matendo fulani. Hapa, mwandishi ametaja tendo linalotekelezwa na kutoa mfano wa wimbo unaoimbwa. Baada ya kutoa mfano wa wimbo, anauchanganua na kubainisha maudhui yaliyomo. Maudhui yanayowasilishwa yanaonesha mchakato mzima wa utendaji wa tohara kuanzia siku ya kwanza hadi ya tatu, wakati ambapo utendaji wa tohara yenyewe hukamilika. Nyimbo ambazo zimenukuliwa zinaonesha mambo kama vile: matayarisho ya tohara, vijana kuzuru ugenini, vijana kuondoka ugenini, vijana kujipa hamasa, na vijana kuondolea jamaa zao wasiwasi.</p> Wanyenya Willy Copyright (c) 2021 https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/13 Tue, 05 Oct 2021 00:00:00 +0000 HADHIRA YA USHAIRI HURU WA KISWAHILI NI IPI? https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/8 <p style="text-align: justify;">Makala hii inaangazia mustakabali wa hadhira katika upokezi wa ushairi huru wa Kiswahili. Mwanzoni mwa miaka 1970, ushairi huu ulijitokeza kwa kasi na ulituhumiwa kwa kutozingatia arudhi za kimapokeo. Watunzi wa awali wa ushairi huu walikuwa wataalamu wa lugha na wahakiki wa fasihi; waliotoa maelezo muhimu kuhusu dhana na sifa za ushairi wa Kiswahili. Kabla ya miaka 1960, ushairi wa kimapokeo ulikuwa umesambaa na umezoewa katika jamii. Kujitokeza kwa ushairi huru kulisababisha watunzi na hadhira kugawanyika katika makundi: lile linalojinasibisha na arudhi, lile lisilojinasibisha na arudhi, na lile linalojinasibisha kwa kiasi na arudhi hizo. Katika miaka ya 1970, waliouendeleza zaidi ushairi huru walikuwa ‘vijana’ waliobahatika kupata elimu ya juu katika taaluma ya fasihi na walitarajia kuchangia katika ufafanuzi wa dhana na sifa za ushairi wa Kiswahili kwa ujumla. Swali linalofafanuliwa katika makala hii ni: kwa nini ushairi huru wa Kiswahili ni kivutio cha wataalamu wa lugha na wahakiki wa fasihi? Nadharia ya Semiotiki imetumika kufafanulia matini za lugha kama viishara na viashiria vinavyohitaji kufasiriwa. Data ya uchanganuzi ilitokana na upitiaji wa mashairi katika diwani teule za mashairi ya Kiswahili. Aidha, data nyingine ilitokana na usaili na hojaji kwa wanafunzi wa vyuo vikuu na wataalamu wa lugha na fasihi.</p> Joseph N. Maitaria Copyright (c) 2021 https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/8 Tue, 05 Oct 2021 00:00:00 +0000 UFUNDISHAJI NA UJIFUNZAJI WA MOFOLOJIA PAMOJA NA UMILISI WA KIWANGO CHA CHINI MIONGONI MWA WANAFUNZI WA VYUO VIKUU NCHINI UGANDA https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/10 <p>Ufundishaji na ujifunzaji wa masomo ya isimu katika lugha ya&nbsp;&nbsp; Kiswahili vyuoni umeathiriwa na changamoto kadhaa. Miongoni&nbsp;&nbsp; mwazo ni matumizi ya misamiati ya kisayansi ambayo imeathiri&nbsp;&nbsp; upataji na ukuaji wa umilisi wa taaluma za kiisimu. Makala hii&nbsp;&nbsp; inalenga kufafanua dhana muhimu katika uchunguzi na uchambuzi wa&nbsp;&nbsp; mofolojia, kuonesha changamoto za ujifunzaji na ufundishaji wake, na&nbsp;&nbsp; kutoa mapendekezo ya kuondokana na changamoto hizo kwa&nbsp;&nbsp; wanafunzi wa vyuo vikuu nchini Uganda na kwingineko. Data&nbsp;&nbsp; ilikusanywa kupitia kwa mijadala shirikishi na usaili kutoka kwa&nbsp;&nbsp; wanafunzi 70 na walimu 9 wa isimu walioteuliwa kimaksudi kutoka&nbsp;&nbsp; katika vyuo vikuu vitatu nchini Uganda. Matokeo yaliyoelezwa kwa&nbsp;&nbsp; muundo wa kimaelezo yalidhihirisha changamoto za kiisimu na zisizo&nbsp;&nbsp; za kiisimu zilizoathiri upataji wa umilisi wa somo la mofolojia. Nazo&nbsp;&nbsp; ni pamoja na: umilisi wa chini katika matumizi ya Kiswahili sanifu,&nbsp;&nbsp; ugumu na kukanganywa katika kueleza dhana za kimofolojia,&nbsp;&nbsp; mitazamo hasi, pamoja na uchache wa vitabu vya isimu vinavyokidhi&nbsp;&nbsp; masilahi ya wanafunzi wa viwango vyote vya umilisi. Utafiti&nbsp;&nbsp; ulipendekeza kuwapo kwa mijadala na makongamano, uandishi wa&nbsp;&nbsp; vitabu mwafaka vya isimu, na kujenga uchanya wa ujifunzaji wa somo&nbsp;&nbsp; la mofolojia.</p> Mulei Martin Copyright (c) 2021 https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/10 Tue, 05 Oct 2021 00:00:00 +0000 UCHANGANUZI WA UBADILISHAJI NA UCHANGANYAJI MSIMBO KATIKA NYIMBO ZA ASILI NCHINI TANZANIA: MIFANO KUTOKA KATIKA NYIMBO ZA KABILA LA WAMATENGO https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/2 <p>Makala hii inafafanua uchanganyaji msimbo na ubadilishaji msimbokatika nyimbo za asili ya kabila la Wamatengo nchini Tanzania. Kutokana na jamii nyingi kuwa na hali ya uwililugha au wingi lugha, mara nyingi, wazungumzaji huchagua msimbo wa kutumia kutegemeana na mazingira au sababu nyinginezo. Uchaguzi wa msimbo hupelekea wazungumzaji kuchanganya au kubadili msimbo. Makala hii inatokana na utafiti ulioongozwa na nadharia ya uwililugha. Jumla ya nyimbo 25 zilikusanywa na kufanyiwa uchunguzi. Pia, wahojiwa watano walishirikishwa ili kupata sababu za uchanganyaji na ubadilishaji msimbo katika nyimbo. Data zimewasilishwa kwa kila wimbo na kutolewa maelezo yanayofafanua vipengele vya uchanganyaji kama vile mofimu, maneno, virai, vishazi na sentensi pamoja na sababu za uchanganyaji au ubadilishaji huo.</p> Fokas Mkilima Copyright (c) 2021 https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/2 Tue, 05 Oct 2021 00:00:00 +0000 USAWIRI CHANYA WA WATOTO KATIKA FASIHI YA WATOTO KAMA NJIA FAAFU YA KUJENGA JAMII BORA YA LEO NA KESHO: MIFANO KUTOKA VITABU TEULE VYA WATOTO VYA KISWAHILI https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/5 <p>Mshengyezi (2003) anadai kuwa, fasihi siyo tu matokeo ya matendo ya wanajamii, bali pia, ni wakala mzuri wa kuipa jamii mwelekeo mzuri kama ikisawiri mambo vizuri na ikatumiwa vizuri. Memmi (2006) anasisitiza kuwa waandishi wa fasihi wana chombo muhimu sana mikononi mwao ambacho kutokana na ubunifu wao, huwawezesha wasomaji kuamini na kuathirika kutokana na kile wanachokisoma au kusikiliza. Memmi (keshatajwa) anaongeza kuwa hata kama kazi fulani ya fasihi ni ya kubuni, bado wahusika wake wanaweza kubebeshwa mawazo ya waandishi kuhusiana na jinsi ambavyo wasanii huyaona maisha na jinsi wanavyotamani maisha hayo yawe. Hivyo, yeye anahitimisha kwa kusema kuwa, fasihi ni chanzo muhimu sana cha ujenzi wa taifa endelevu. Lengo huu la makala hii ni kushadidia hoja kwamba, fasihi ya watoto ikiwasawiri vyema watoto na kuwaonesha kuwa ni watu muhimu, tunaweza kuwa na jamii bora leo na kesho. Makala inachambua na kubainisha hoja zake kwa kutumia kazi kumi na moja za Kiswahili zilizoandikwa kwa ajili ya kusomwa na watoto. Makala inaongozwa na Nadharia za Usimulizi na Kisosholojia. Katika matokeo ya uchambuzi wa data, inabainika kwa uwazi kwamba, watoto wanaposoma, huamini yale wanayoyasoma; hivyo kuwa na uwezekano mkubwa wa kubadilishwa na kile wanachokisoma. Hivyo, kama tukichukua tahadhari tukawasawiri vyema watoto, kama asemavyo Memmi (2006), tunayo nafasi kubwa ya kuwaathiri vizuri watoto ili wajenge jamii nzuri.</p> Leonard H. Bakize Copyright (c) 2021 https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/5 Tue, 05 Oct 2021 00:00:00 +0000 CHANGAMOTO ZA UINGIZWAJI WA MASUALA YAHUSUYO LUGHA KATIKA SERA ZA ELIMU NA UTAMADUNI: HAJA YA KUWA NA SERA MAHUSUSI YA LUGHA TANZANIA https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/11 <p>Makala hii inajadili changamoto mbalimbali zinazohusiana na sera ya lugha. Kwa muda mrefu, nchi ya Tanzania haina sera mahususi ya lugha, badala yake, masuala ya lugha yameingizwa katika Sera ya Utamaduni na Sera ya Elimu. Sera ya lugha ni jumla ya mawazo, matamko, sheria, kanuni na taratibu zenye kufafanua utekelezaji wa mabadiliko ya matumizi ya lugha (Mekacha, 2000; na Msanjila, 2009). Aidha, makala inafafanua kuhusu dhana, aina ya sera za lugha, na kuonesha namna sera ya lugha kama ilivyoingizwa katika Sera ya Utamaduni na Elimu. Data katika makala hii, kwa kiasi kikubwa, zimekusanywa kutoka maktaba na kwa wadau mbalimbali wa lugha. Changamoto zilizojadiliwa ni pamoja na: kutokuainishwa kwa mpango wa utekelezaji wa sera, sera ya lugha kushughulikia suala la elimu tu, na kutokupewa nafasi ya lugha nyingine za jamii. Mintarafu ya changamoto hizo, makala imebainisha sababu za changamoto hizo. Pia, imebainisha umuhimu kuhusu haja ya kuwa na sera madhubuti na mahususi ya lugha nchini Tanzania.</p> Ahmad Y. Sovu Copyright (c) 2021 https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/11 Tue, 05 Oct 2021 00:00:00 +0000 UFUNDISHAJI NA UJIFUNZAJI KATIKA NYUGA ZA KIINSIA: HATARI ILIYOPO INAKABILIWA? https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/9 <p>Makala hii inakusudia kubainisha hatari inayozikabili nyuga za kiinsia. Hatari hiyo sio nyingine bali ni nyuga za kiinsia kupoteza umuhimu wake. Miongoni mwa ithibati ya kuwapo kwa hatari hii ni pamoja na idara mbalimbali za nyuga za kiinsia katika vyuo vikuu mbalimbali kufungwa. Aidha, katika nchi zinazoendelea, idadi ya&nbsp;&nbsp; udahili kwa wanafunzi wa nyuga za kiinsia imeshuka sana. Hii ni kutokana na serikali za nchi husika kupunguza au kuondosha kabisa ufadhili kwa wanafunzi hao. Makala imeonesha sababu za nyuga za&nbsp;&nbsp; kiinsia kuonekana kupoteza umuhimu wake kuwa ni pamoja na maendeleo na mabadiliko ya kiuchumi yaliyosababisha thamani za nyuga kupimwa zaidi kwa faida za kiuchumi. Aidha, makala imeonesha namna ambavyo utetezi unaotolewa na wadau wa nyuga za kiinsia ambavyo umeonekana kutegemea zaidi huruma kuliko&nbsp;&nbsp; kudhihirisha namna ambavyo nyuga za kiinsia bado zina nafasi ya kufanikisha faida za kiuchumi. Hivyo basi, makala imeweka wazi sifa za wafanyakazi, maarifa yatakiwayo, na stadi zinazohitajika katika zama hizi za kidijiti. Hii imefanyika ili kutoa fursa kwa walimu, wataalamu, na wadau wengine wa nyunga za kiinsia, hususani katika vyuo vikuu, wapate nafasi ya kujifanyia tathimini iwapo kweli&nbsp;&nbsp; michakato yao ya ufundishaji na ujifunzaji inakabiliana na hatari hii iliyopo. Mwisho, makala inamalizia kwa kutoa mapendekezo ya nini&nbsp;&nbsp; kinapaswa kufanyika.</p> Wallace K Mlaga Copyright (c) 2021 https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/9 Tue, 05 Oct 2021 00:00:00 +0000 ATHARI ZA MFUMO WA VIHUSISHI VYA KINANDI KATIKA UAMILIAJI WA KISWAHILI KAMA L2 MIONGONI MWA WANAFUNZI WANAOSEMA KINANDI KAMA L1 https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/6 <p>Uamiliaji wa L2 ni tukio lisiloepukika katika karne ya sasa yenye migusano mingi&nbsp; ya lugha inayosababishwa na mitagusano ya watu wanaosema lugha tofauti na&nbsp; kupitia ujifunzaji na ubwiaji wa lugha. Uamiliaji wa L2 ni zao la maendeleo ya&nbsp; binadamu, kijamii, kiuchumi na kisiasa. Maendeleo haya hulazimisha nchi na watu&nbsp; kujifunza lugha nyingine ili mahitaji fulani ya maendeleo yaweze kuafikiwa.&nbsp; Uamilijia huu unakuwa wa lazima ili watu wanaosema lugha tofauti waweze&nbsp; kuelewana na kubadilishana mawazo. Mwamiliaji wa L2 mara nyingi hukumbwa na&nbsp; changamoto ya kuathiriwa na mfumo wa kiisimu wa LI. Athari kutoka L1 ni za&nbsp; kifonetiki, kifonolojia, kimofolojia, kisintaksia na kisemantiki, ambazo&nbsp; zinamwaathiri mwamiliaji wa L2. Makala hii imeshughulikia athari za&nbsp; kimofosintaksia za mfumo wa vihusishi vya Kinandi katika insha za Kiswahili za&nbsp; wanafunzi wanaosema Kinandi kama L1. Ni zao la utafiti uliofanywa katika shule&nbsp; tatu za msingi katika Kaunti ya Nandi nchini Kenya kwa minajili ya kuandaa tasnifu&nbsp; ya uzamili. Katika utafiti huo, shule hizi zilirejelewa kwa akronimu NSB. Utafiti huo&nbsp; ulibainisha changamoto nyingi za kiisimu-nafsia katika kiwango cha&nbsp; kimofosintaksia zinazomkumba mwanafunzi anayesema Kinandi kama L1&nbsp; anapoamilia Kiswahili kama L2. Mojawapo ya vyanzo vya changamoto hizi ni&nbsp; athari za mfumo wa vihusishi vya Kinandi zinazojadiliwa katika makala hii.</p> Susan Chebet-Choge Copyright (c) 2021 https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/6 Tue, 05 Oct 2021 00:00:00 +0000 UFUTUHI WA KIAFRIKA: NADHARIA MPYA YA KUSHUGHULIKIA TAALUMA ZA KI-INSIA https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/12 <p>Makala hii inawasilisha jaribio la kuifafanua nadharia ya Ufutuhi wa&nbsp;&nbsp; Kiafrika kama nadharia mpya yenye uwezo wa kutumika kushughulikia masuala ya ki-insia. Taaluma za ki-insia, katika makala hii, zinamaanisha shughuli kama vile tafiti na tahakiki zinazofanywa kwenye nyuga zinazohusiana na lugha, sanaa, historia, falsafa, na utamaduni. Kwa kipindi kirefu, taaluma kama hizi zinazowahusu Waafrika zimekuwa zikishughulikiwa kwa kutumia viunzi vya nadharia vyenye asili na mwegamo wa maeneo ya nje ya jamii za Kiafrika. Hali hii, kwa namna moja au nyingine, husababisha upungufu katika kupata majibu ya matatizo yanayoshughulikiwa. Katika kuitikia wito kwa wanataaluma wa Kiafrika kutafuta na kutumia nadharia zenye asili na mwegamo wa jamii husika, makala hii inaitambulisha dhana ya Ufutuhi wa Kiafrika kama nadharia yenye uwezo wa kuwa Kiunzi cha Nadharia8 chenye uwezo wa kuendeshea taaluma za ki-insia.</p> Athumani S. Ponera Copyright (c) 2021 https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/12 Tue, 05 Oct 2021 00:00:00 +0000