JARIDA LA MNYAMPALA https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala <p><strong>Jarida la Mnyampala (JM)</strong> ni jarida la kitaaluma lililopo chini ya idara ya Kiswahili ya Chuo Kikuu cha St John’s cha Tanzania. JM limesajiliwa na Maktaba Kuu ya Taifa mwaka 2019 na kupewa namba ya usajili ISSN 2683-6440 (nakala ngumu [print]) na e-ISSN 2683-6432 (nakala tepe ya mtandaoni [online]). Jarida limejikita katika uchapishaji wa makala za Fasihi, Isimu na Utamaduni wa Kiswahili. Hivyo basi, waandishi, watafiti na wapenzi wa Kiswahili wanakaribishwa kuchapisha makala katika jarida hili. Makala zote zitumwe kwa mhariri mkuu kupitia baruapepe <strong>jaridalamnyampala@sjut.ac.tz.</strong></p> en-US JARIDA LA MNYAMPALA 2683-6440 SAUTI YA DHIKI: HAZINA YA KUHIFADHI, KUKABILI NA KUFUATILIA MAOVU YOTE KWA NJIA YA AMANI https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/28 <p><em>Kenya imepitia kipindi kisicho mfano cha kukiukwa kwa haki za binadamu. Hili limedhihirika kupitia migogoro na mizozo ya mara kwa mara ya kikabila. Ukiukwaji huu unajumuisha mauaji ya halaiki, mateso, uovu, pamoja na uhalifu wa aina mbalimbali. Kwa kuzingatia ukweli huu, wasanii, wakiwemo washairi, pia wanajitokeza kuchangia katika suala hili. Kwa kutumia diwani ya Sauti ya Dhiki (Abdalla, 1973), makala hii inatalii jinsi dhuluma na kususia huwasilishwa kishairi. Ushairi wa Kiswahili unajitokeza kama chombo cha kuangazia dhuluma mbalimbali za kijamii na za kisiasa na kama njia ya kuelezea hisia za kibinafsi kuhusu dhuluma. Ushairi unasomwa kama njia ya kuwawezesha watu kuasi na kupinga hali na mifumo inayowakandamiza, kuwasilishia yasiyowasilishika, na kutoa sauti mbadala ya kuelezea masuala yanayoisakama jamii.</em></p> <p><em>&nbsp;</em><strong>Lugha na Sanaa ya Kusema </strong><strong>“La</strong><strong>! </strong><strong>kwa Ukatili” </strong></p> <p>Historia ya Kenya imejaa visa vya mauaji ya kutisha ambayo baadhi yake yanasemekana kuwa yalifadhiliwa na vyombo vya usalama kwa kisingizio cha oparesheni ya usalama. Kwa mujibu wa Ripoti ya Tume ya Haki na Maridhiano, utawala wa serikali mbalimbali umechukuliwa kuwa mwendelezo wa ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu (TJRC, 2013). Ukiukaji huu umejitokeza kupitia vita<sup>3</sup>, mauaji<sup>4</sup>, mateso<sup>5</sup>, adhabu ya pamoja, kumnyima mtu mahitaji ya msingi, mauaji ya kisiasa,<sup>6</sup> kutia mtu kizuizini, dhuluma pamoja na unyanyasaji wa wapinzani wa kisiasa na wanaharakati wa haki za binadamu. Orodha hii ndefu ya visa vya ukatili imevuta makini ya washairi ambao wana jukumu la kuwa sauti ya mnyonge. Uchunguzi wa tungo za fasihi ya Kiswahili unaonyesha matukio ambapo Waswahili walitumia sanaa zao kudai uhuru wao wa kisiasa na wa kiuchumi. Ushairi ulijitokeza kama njia ambayo kwayo msanii aliwapatia sauti ‘wanaoteswa’ (Dawes, 2007). Makala hii inafafanua jinsi suala hili la ukatili lilivyoangaziwa katika <em>Sauti ya Dhiki</em>. Diwani hii ilitungwa na Abdilatif Abdalla baada ya ukoloni nchini Kenya. Ingawa hii ni diwani ya mwandishi mmoja tu, ina data za kutosha</p> <hr align="left" width="30%"> <p><sup>3 </sup>Mifano ni pamoja na vita vya Maumau na vya Mashifta.</p> <p><sup>4 </sup>Haya ni pamoja na mauaji ya Kedong, Ususiaji wa Giriama, Mauaji ya Kollowa, ya Lari, ya Hola, ya Turbi na ya Bubisa (2005), ya Murkutwa (2001), ya Loteteleit (1988), ya Bulla Karatasi (1980), ya Wagalla, (1984), ya Lotirir (1984) ya Malka Mari (1981), na ya Garissa (1980).</p> <p><sup>5 </sup>Hasa vyumba katika majengo ya Nyayo na Nyati vilivyotumiwa kuwatesa wapinzani.</p> <p><sup>6 </sup>Waliouawa ni pamoja na Pio Gama Pinto, Tom Mboya, J.M. Kariuki, Dr. Robert Ouko, Askofu Alexander Muge Crispine Odhiambo Mbai, na Padri John Kaiser.</p> Nahashon A. Nyangeri Hassan R. Hassan Copyright (c) 2024 2020-06-30 2020-06-30 1 1 12 FASIHI YA KISWAHILI: MUSTAKABALI WA TANZANIA KATIKA MUKTADHA WA UTANDAWAZI https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/31 <p>Wanazuoni wengi wa ndani na nje ya Afrika wanatumia mbinu mbalimbali za kisanaa ili kueleza masuala yanayosawiri hali halisi iliyopo katika mataifa yao. Baadhi ya masuala yanayoelezwa ni pamoja na kutamalaki kwa utandawazi na athari zake katika mataifa yanayoendelea. Makala hii imeeleza nafasi ya fasihi ya Kiswahili katika kuimarika kwa utandawazi katika nchi za Kiafrika kwa kipindi cha miongo mitatu iliyopita. Katika kipindi hiki, mataifa ya Kiafrika yameshuhudia mapinduzi makubwa katika mifumo ya siasa na sera za uchumi huria unaodhibitiwa na mataifa ya kibepari. Kwa hiyo, makala hii imechunguza athari za utandawazi nchini Tanzania kwa kurejelea riwaya teule za Bina-Adamu (2002) ya K. W. Wamitila na Msomi Aliyebinafsishwa (2012) ya N. Nyangwine. Riwaya hizi zimeteuliwa kwa kuwa zinaakisi vizuri hali halisi ya harakati na athari za utandawazi hapa nchini. Pia, inadokeza mustakabali wa Tanzania ya sasa na ijayo. Data za makala hii zilipatikana maktabani. Nadharia ya Uhalisia imetumika katika uchambuzi na mjadala wa data zilizowasilishwa. Makala inahitimisha kuwa kadiri harakati za utandawazi zinavyozidi kuimarika nchini, ndivyo mifumo ya kiutamaduni, kisiasa na kiuchumi inavyozidi kudhoofika na kuporomoka.</p> Gerephace Mwangosi Mussa, E. Msamilah Copyright (c) 2024 2020-06-30 2020-06-30 1 13 25 UTAMADUNI WA MZANZIBARI: MILA NA DESTURI KATIKA VAZI LA KANGA https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/32 <p>Makala hii inaangazia matumizi ya vazi la kanga katika mila na desturi katika utamaduni wa Mzanzibari. Kila jamii huwa na kaida zake ambazo hutofautiana na jamii nyingine. Kaida hizo huwa katika chakula, mavazi, pamoja na mfumo mzima wa maisha. Lengo la makala hii ni kubainisha kwa namna gani Wazanzibari wanavyotumia kanga kulingana na mila na desturi zao. Matumizi hayo huwa katika hatua mbalimbali za makuzi ya mwanadamu, kuanzia kuzaliwa kwake, kuishi na kufa kwake. Makala hii ni sehemu ya utafiti mkubwa uliofanywa na Saade Mbarouk (2011) ambao unahusu Athari za Semi za Kanga kwa Jamii ya Zanzibar. Ukusanyaji wa data ulifanywa kwa kutumia mbinu ya mahojiano. Nadharia ya Naratolojia imetumika katika kuchambua data. Katika makala hii waandishi wameeleza fasili ya kanga, aina za kanga, asili ya jina la kanga pamoja na historia ya kanga. Mwisho, wameelezea umuhimu wa kutunza utamaduni wa jamii.</p> Saade S. Mbarouk Ulfat A. Ibrahim Copyright (c) 2024 2020-06-30 2020-06-30 1 26 37 DHIMA YA TAFSIRI HIFADHI: UCHUNGUZI WA BIBLIA TAKATIFU https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/33 <p>Makala hii inafafanua dhima ya tafsiri hifadhi katika Biblia. Msingi wa makala hii ni kubainisha, kuchambua na kueleza dhima ya maneno ya lugha chasili ambayo yameendelea kuwapo katika Biblia hadi sasa. Maswali yanayoongoza makala hii ni mawili. Je, maneno yapi katika Biblia ni ya lugha chasili? Kwa nini maneno hayo yaendelee kuwapo katika lugha lengwa, hasa Kiswahili? Methodolojia ya utafiti huu ni uchanganuzi wa maneno yaliyopo katika tiniwayo katika Biblia: Maandiko Matakatifu toleo la mwaka 1997. Makala inabainisha kwamba tafsiri hifadhi ina dhima kubwa, hasa katika Biblia. Aidha, matokeo ya uchambuzi wetu yanaonesha kwamba tafsiri hifadhi, pamoja na dhima nyinginezo, inatunza utukufu wa Kimungu, historia na kumbukumbu ya mambo mbalimbali na kuonesha msisitizo wa mambo ya Kimungu. Kutokana na matokeo haya, makala hii inapendekeza kwamba, wasomaji wa tafsiri hifadhi wajijuvye vya kutosha kuhusu masalia ya lugha chanzi yaliyomo katika matini lengwa, hususani Biblia, ili waweze kuelewa ujumbe uliomo katika matini husika. Wasomaji hawa wataweza kujijuvya dhima za masalio yaliyopo katika maandiko kupitia kamusi, kusoma maandiko mengine yenye welekeo moja na kuwakabili wazungumzaji wa lugha chanzi.</p> Rehema Stephano Emanuel Samwel Kaghondi Copyright (c) 2024 2020-06-30 2020-06-30 1 38 49 MATUMIZI YA LUGHA YA KISWAHILI KATIKA MFUMO WA HUDUMA ZA AFYA NCHINI TANZANIA: MJADALA WA MWEGAMO NA MAWANDA YAKE https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/34 <p>Makala hii ni sehemu ya ripoti ya mradi wa utafiti mpana uliofanyika mwaka 2018/19 katika mikoa mitano ambayo ni Lindi, Kilimanjaro, Dar es Salaam, Kagera na Kaskazini Pemba. Utafiti huo ulifadhiliwa na Chuo Kikuu cha Dodoma. Utafiti ulihusu suala la matumizi ya lugha ya Kiswahili katika duara zima la utoaji wa huduma za afya. Watoa taarifa katika utafiti huu walikuwa: wanataaluma wa taaluma za afya, watoa huduma, wapewa huduma na viongozi wa sekta ya afya. Data zilikusanywa kupitia njia za udodosaji, usaili, na mijadala ya vikundi lengwa. Makala hii inahusu mwegamo wa matumizi ya lugha ya Kiswahili katika utoaji wa huduma za afya nchini Tanzania pamoja na mawanda yake. Makala ina sehemu nne mbazo ni: Utangulizi, mwegamo wa matumizi ya Kiswahili katika utoaji wa huduma za afya, mawanda ya matumizi ya Kiswahili katika utoaji wa huduma za afya pamoja na hitimisho.</p> Athumani S. Ponera Abdallah Baja Getruda Shima Tatu Y. Khamis Leah Kiloba Copyright (c) 2024 2020-06-30 2020-06-30 1 50 61 DHANA YA UHUSIKA KATIKA KAULI YA KUTENDEA https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/35 <p>Dhana ya uhusika ina utata katika machapisho wa Kiswahili. Hii ni kwa sababu wakati mwingine ikifasiliwa kuwa ni dhana ya kimuundo, na wakati mwingine, ni dhana ya kisemantiki. Makala hii inapendekeza kuichukulia dhana hiyo kuwa ni ya kimuundo na dhana ya ushiriki kuwa ni ya kisemantiki. Dhana hizo mbili zinaelezwa kwa kutumia mifano kutoka kauli ya kutendea. Unyambulishaji wa kutendea husababisha kitenzi kupata yambwa mpya. Yambwa mpya inaweza kutafsiriwa kwa namna mbalimbali kutokana na uhusiano wa yambwa hiyo na kitenzi. Kwa kutumia uhusiano mbalimbali wa yambwa na vitenzi, inaonesha kwamba uhusika wa ala waweza kuwa wa namna mbalimbali. Ushahidi unaotokana na uchambuzi wa sentensi za utendea na yambwa mbadala unadhihirisha kwamba tofauti za ushiriki zinatokana na maana ya mzizi wa kitenzi na hulka za nomino ninazohusika katika matukio.</p> Deo Ngonyani Copyright (c) 2024 2020-06-30 2020-06-30 1 62 77 MTANGAMANO KAMA KIUNGO CHA MSHIKAMANO KATIKA DISKOSI ZA KIWINGI-LUGHA https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/36 <p>Mshikamano ni elementi muhimu ya kiisimu inayochangia ufasili wa maana katika diskosi. Makala hii, hivyo basi, inafafanua jinsi mtangamano unavyohusika kama kiungo cha mshikamano katika diskosi za kiwingi-lugha. Nadharia Amilifu Zalishi ilitumiwa katika uchunguzi huu (Sawe, 2015). Nadharia hiyo inasisitiza kwamba uunganishaji, uradidi na mtangamano ni mikakati inayojenga mshikamano katika matini au diskosi huku ikipinga dai kwamba udondoshaji ni kijenzi cha mshikamano. Data ilikusanywa kutoka sampuli ya makanisa mawili na vyuo vikuu viwili nchini Kenya. Diskosi za kiwingi-lugha za wanafunzi waliozungumza Kiswahili, Kikipsigis na Kiingereza zilichunguzwa. Utafiti huu uligundua kwamba wanawingi-lugha hutumia mtangamano kama mojawapo ya mikakati ya kuendeleza mshikamano katika mazungumzo yao yenye ubadilishaji msimbo.</p> Salim Sawe Mosol Kandagor Copyright (c) 2024 2020-06-30 2020-06-30 1 78 89 MIKAKATI, CHANGAMOTO NA MUSTAKABALI WA UTUNGAJI WA KAMUSI ZA KIISTILAHI ZA KISWAHILI https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/37 <p>Maendeleo katika taaluma ya leksikografia yamepelekea kuwapo kwa idadi kubwa ya kamusi za istilahi za Kiswahili katika nyanja za taaluma mbalimbali. Hata hivyo, licha ya maendeleo hayo, hakuna kamusi kamilifu isiyo na upungufu wa aina fulani. Kwa kutumia mbinu za utafiti wa maktabani, makala hii imefafanua mikakati, changamoto na mustakabali wa utungaji wa kamusi za kiistilahi za Kiswahili. Lengo lake ni kubainisha mbinu zinazofaa zaidi katika utungaji kamusi za istilahi za Kiswahili zitakazokidhi mahitaji ya lugha hiyo katika kipindi hiki na siku za usoni. Hoja kuu ya makala hii ni kwamba kuegemea zaidi kwenye mbinu za tafsiri na zile za kileksikografia badala ya zile za kiteminografia katika utungaji wa kamusi za istilahi za Kiswahili kumetinga ufanisi katika sayansi na sanaa hiyo. Data iliyotumika ni mifano ya istilahi za kompyuta zilizoorodheshwa kama vidahizo katika Kamusi Sanifu ya Kompyuta (Kiputiputi, 2011). Imedhihirika kwamba ubora au upungufu wa kamusi ya kiistilahi hutegemea maumbo ya vidahizo vilivyomo, fasili zake, uzingatiaji wa mifumo na vikoa vya dhana na muundo wa vitomeo vyake. Kwa hivyo, kamusi za kiistilahi za siku za baadaye zitakuwa na mwelekeo wa kuwa mediatutiko, mkondoni na zenye uwezo kusasaishwa kuendana na maendeleo katika uwanja wa taaluma inayohusika.</p> Stanley Adika Kevogo James Omari Ontieri Jackline Njeri Murimi Copyright (c) 2024 2020-06-30 2020-06-30 1 90 104 MATATIZO YA UFUNDISHAJI WA SINTAKSIA KATIKA VYUO VIKUU NCHINI TANZANIA https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/38 <p>Kuanzia miaka ya mwishoni mwa karne ya 20 hadi leo, ufundishaji wa sintaksia umekumbwa na matatizo makuu mawili: (1) nadharia za kufundisha, na (2) maarifa na stadi ambazo mhitimu wa shahada ya kwanza anapaswa kuwa nazo. Makala hii inajadili matatizo haya katika muktadha wa ufundishaji wa sintaksia katika Idara za Kiswahili, vyuo vikuu vya Tanzania. Makala inajadili matatizo haya kwa kuhusisha pia changamoto ya uchanganyaji wa mikabala ya ufundishaji. Katika kujadili matatizo haya yote, makala inabainisha kwamba changamoto hizi za ufundishaji wa sintaksia zinatokana na sababu kuu mbili: (1) uhaba wa wataalamu wa sintaksia katika ngazi husika; na (2) kukosekana kwa jukwaa au “chombo” kinachoweza kusimamia mijadala kuhusu nadharia, mikabala na maarifa yanayopaswa kuzingatiwa katika ufundishaji wa sintaksia/isimu kwenye vyuo vikuu. Miongoni mwa mapendekezo yanayotolewa ni kuwapo kwa chombo cha uratibu kitakachosimamia ufundishaji wa isimu ya Kiswahili katika vyuo vikuu, si nchini Tanzania tu, bali kwenye vyuo vikuu vyote vya Afrika Mashariki. Kwa kuwa tayari kuna vyombo kadhaa (kama vile CHAKAMA-TZ na TATAKI), kimojawapo cha vyombo hivyo kinaweza kupewa jukumu hilo kama ikionekana inafaa.</p> Kulikoyela K. Kahigi Fabiola Hassan Copyright (c) 2024 2020-06-30 2020-06-30 1 105 121 MATUMIZI YA LUGHA YA VIJANA KWA WANAFUNZI WA SHULE ZA SEKONDARI TANZANIA https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/39 <p>Makala hii imejadili matumizi ya lugha ya vijana wa shule za sekondari nchini Tanzania, na mambo yanayosababisha matumizi hayo. Cheshire (1982) na Milroy (1978, 1987) wanaeleza kuwa utofauti wa lugha hutokana na mahusiano yaliyopo katika kundi linalohusika ambapo hutegemea mila, desturi, na kaida ambazo hufanana katika kundi hilo na kufanya kuwapo kwa matumizi tofauti ya lugha katika matamshi, msamiati na tungo. Makala hii imetumia data kutoka uwandani zinazohusu matumizi ya lugha ya vijana wa sekondari wilaya ya Morogoro. Nadharia ya Milroy (1980) inayohusu mitandao ya kijamii imetumika kuchambua data hizo. Makala hii imebaini kuwa vijana wa sekondari wana matamshi, msamiati na tungo wanazozitumia katika mazungumzo yao ambazo hutofautiana na zile za marika mengine. Hali hii husababishwa na haja ya kuwa na usiri au kuficha maana iliyokusudiwa, ucheshi na utani, kuonesha mshikamano na mazoea yaliyojengeka miongoni mwao.</p> Faraja Mwendamseke Saul Bichwa Copyright (c) 2024 2020-06-30 2020-06-30 1 122 131 NGONJERA NA MTAZAMO MPYA WA MALEZI YA WATOTO NA VIJANA https://journals.sjut.ac.tz/index.php/mnyampala/article/view/40 <p>Malezi ya watoto na vijana kwa jumla ni ada muhimu katika ustawi wa jamii yoyote inayohitaji kupiga hatua za kimaendeleo. Isivyo bahati, jamii imeshughulishwa mno masuala mengine ya kimaisha, na kuwaacha watoto na vijana wajilee wenyewe. Wakati haya yakitokea, waandishi wawili— Ramadhan Nyembe na Abdallah Seif—wanajitokeza kuikumbusha jamii kuhusu ulezi wa watoto na familia kupitia ngonjera. Makala hii inachambua mchango wa wasanii hawa wa ngonjera katika kuirejesha jamii katika mstari wa malezi kupitia tungo zao mbili, Ngonjera Elimishi Na.1 na Ngojera: Nasaha na Uzalendo. Uchambuzi wa matini umetumika kama njia ya kupata taarifa mbalimbali za kitabuni. Aidha, nadharia ya uhalisia imetuongoza katika uchambuzi na uwasilishaji wa taarifa mbalimbali za kitabuni. Hii ni kusema kuwa, mambo mengi yaliyozungumzwa na waandishi ni mwangwi wa maisha halisi yanayojitokeza katika jamii. Ili kufikia lengo la makala hii, mwandishi ameshughulikia ngonjera zinazohusiana na malezi ya watoto na vijana tu. Kwa jumla, wasanii wameweza kufikisha ujumbe muhimu kwa jamii. Wamezungumzia mambo muhimu kama vile umuhimu wa elimu kwa watoto, madhara ya pombe na dawa za kulevya, imani za kishirikina na heshima kwa wakubwa.</p> Shadidu Abdallah Ndossa Copyright (c) 2024 2020-06-30 2020-06-30 1 132 145